Top News

Sunday, March 31, 2013

MUDA USIOZIDI MIEZI 12 WEMA SEPETU ATUMIA ZAIDI YA MILION 800

SHIKAMOO Wema! Shikamoo dada Wema! Ndiyo iliyokuwa salamu na topiki kwenye mitandao ya kijamii wiki iliyopita.
Ilikuwa ni baada ya wewe mwigizaji kinara wa filamu za nyumbani, Wema Isaac Sepetu kumnusuru staa mwenzako, Kajala Masanja.
Kweli ulimuokoa kwenda jela miaka saba kwa kumlipia faini ya Sh. milioni 13 za madafu.
Kama ulikosa muda wa kupitia maoni katika mitandao ya kijamii, nitakwambia. Maoni yalikuwa mengi hasa yale ya kukusifia. Wengine walikuita dada, wengine mama pamoja na kwamba wamekupita kiumri.
Kweli Wema umelitendea haki jina lako kwa kutenda wema kwa wengine japo leo nitakupa matukio yako ya kufuru katika kipindi kifupi kisichozidi miezi kumi. Kufuru zote ulianza Juni, mwaka jana na tayari umeteketeza zaidi ya Sh. milioni 800 katika ghughuli zako. Nitaziorodhesha ‘then’ tutajadili walau kidogo kwa kuwa wewe ni mmoja wa vijana watafutaji.
Kuhusu kufuru zako sishangai kwa kuwa zinahamasisha vijana kutafuta mkwanja. Kama wewe ni mfuatiliaji wa soka la England nitakwambia kitu. Unakumbuka tukio la kufuru ya fedha la aliyekuwa straika wa Manchester City ya England, Mario Balotelli kabla ya kutua AC Milan? Siku moja alinaswa kule England akitapanya Sh. milioni 100 akakamatwa na kufunguliwa mashitaka. Wewe umeona usifanye kama Balotelli. Unafanya yako!
Katika kipindi hicho cha miezi kadhaa umefanya mambo makubwa. Nawatazama matajiri wa Kibongo sioni mwenye makeke kama yako.
Nitakukumbusha! Katikati ya mwaka jana ulitamba kununua nyumba Kijitonyama, Dar kwa Sh. milioni 400. Haikutosha ukaikarabati na kuweka samani kwa Sh. milioni 30.
Wakati wadadisi wa mambo wakimwaga data kuwa ni jeuri ya fedha za mume wa mtu, wewe uliziba masikio, ukazama Dubai ukawaziba midomo kwa shopping ya Sh. milioni 60.
Nakumbuka ulizindua filamu yako ya The Super Star kwa kumleta staa mkubwa wa Nollywood, Nigeria. Gharama zote zilikuwa ni Sh. milioni 40 na kufuatiwa na makeke mengine ya ununuzi wa magari ya bei mbaya. Ulinunua Toyota Lexus Harrier, Sh. milioni 25, Toyota Mark X, Sh. milioni 60 na Audi Q7 la Sh. milioni 80.
Weka mikoko pembeni, uzinduzi wa ofisi yako ya Endless Fame ulikuwa gumzo, taarifa zilieleza kuwa ulitumia zaidi ya Sh. milioni 70. Mengine ni kufuru ya kuwafanyia mbwa wako shopping ya zaidi ya Sh. milioni 6, kumwokoa Kajala asiende jela kwa kumlipia faini ya Sh. milioni 13 na kutunza wasanii wa muziki stejini.
Wema umeendeleza pale mwigizaji Jacqueline Wolper alipoishia. Wewe umemwokoa Kajala, yeye alipigania uhai wa mwigizaji Juma Kilowoko ‘Sajuki’ kwa kumchangia Sh. milioni 16 za matibabu.
Niliwahi kusema hapa kuwa baadhi ya wasanii wetu hawana kasumba ya kujitolea katika jamii. Alichokifanya Wema ni cha kupongezwa lakini sasa tunahitaji wajitokeze wasanii wengine wa kuwasaidia wenzao kama mchekeshaji Said Ngamba ‘Mzee Small’ anayesumbuliwa na ‘stroke’. Yumo pia mwigizaji Juma Salim ‘Mzee Kankaa’ anaumwa baada ya kupata ‘stroke’. Bila kumsahau mwingizaji Ramadhan Mwinshehe ‘Mashaka’ naye kapooza hivyo anahitaji msaada. Ili kujenga jamii yenye kushikamana, si vyema ikajengeka picha kuwa wanaostahili kusaidiwa ni wale wa aina fulanifulani bali ifahamike kuwa kutoa ni moyo na si utajiri. For the love of game!

No comments :

Post a Comment

Designed By ApexbnewZ